.

.

.

.

Monday, January 30, 2012

MADAKTARI KUPOTEZA AJIRA ZAO !!!


BAADA ya madaktari kugomea ombi la Waziri wa Mkuu, Mizengo Pinda kukutana nao jana ili kusikiliza madai yao na kuwasihi wasitishe mgomo, Serikali imetishia kuwafukuza kazi wote watakaoshindwa kuripoti kazini leo huku ikiiagiza Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, kupeleka madaktari wake katika hospitali za mikoa.
Mbali ya hatua hiyo, Serikali pia imepiga marufuku mikusanyiko yote ya madaktari hao na kuliagiza Jeshi la Polisi kuwasambaratisha popote watakapoonekana hatua ambayo imepingwa na madaktari hao ambao nao jana wametoa tamko wakisema watakwenda mahakamani kupinga agizo hilo.
Pinda alisema: “Katika hatua iliyofikiwa, Serikali imetambua kuwa madaktariwanaoongozwa na kamati ya mpito hawataki suluhu licha ya juhudi zote ambazo zimekuwa zikifanywa kuwaita ili kushughulikia madai yao. Kuanzia sasa Serikali inahimiza madaktari wote walio kwenye mgomo kuacha mara moja na kuripoti kazini ifikapo kesho asubuhi (leo), Januari 30, mwaka huu, ”alisema Waziri Mkuu na kuongeza:
“Watakaoshindwa kutekeleza agizo hilo watakuwa wamepoteza ajira zao. Serikali imeshachukua tahadhari za kukabiliana na hali hiyo kwa kuagiza Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa  kupeleka madaktari wake katika Hospitali za mkoa wa Dar es Salaam ili kusaidia wagonjwa walioko hospitalini.”
Madaktari nchini walianza mgomo wao Januari 16, mwaka huu wakitoa madai mbalimbali, ikiwemo kutaka kuongezewa mishahara, posho na kupatiwa nyumba za kuishi.

Januari 25, Pinda akizungumza na wahariri wa vyombo vya habari  ofisini kwake aliwaangukia wanataaluma hao akisema alikuwa tayari kukutana nao wakati wowote lakini, madaktari hao waligoma na kutaka kiongozi huyo awafuate Ukumbi wa Starlight.

Jana, Waziri Mkuu akiwa katika mchakato huo wa kutafuta suluhu ili kunusuru maisha ya wagonjwa katika hospitali zilizokumbwa na mgomo, aliwaalika kukutana nao katika Ukumbi wa Karimjee lakini licha ya kufika hapo akiwa na jopo la mawaziri pamoja na viongozi wengine waandamizi wa Serikali, madaktari hao hawakutokea.
Waliokuwa wameambatana na Pinda tayari kwa mkutano huo ni Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Shamsi Vuai Nahodha, Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk Haji Mponda, Naibu wake Dk Lucy Nkya, Waziri Nchi, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Hawa Ghasia, Katibu Mkuu Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, Blandina Nyoni, Mganga Mkuu wa Serikali, Dk Deo Mtasiwa, na maofisa wengine waandamizi wa Serikali. 

1 comment:

  1. Hao wanajeshi wanatosha kuhudumia mikoa yote au mnataka kutuulia ndugu zetu tu?

    ReplyDelete