.

.

.

.

Wednesday, September 30, 2009

MAJEMBE 3 YA KILONGO HUKO USUKUMANI YENYE MAAJABU

Nilikuwa Shinyanga hivi karibuni na nilitembelea makumbusho ya wasukuma ya Mazingira yaliyopo Shinyanga mjini na kukutana na Museum Curator ambaye alinipa simulizi hili toka kwa watani wangu katika moja ya maswali yangu.Miaka mingi iliyopita majembe haya yamekuwa yakionekana ndani ya mwamba mmoja mdogo kijiji cha Chibe. Majembe haya yako mlimani kando kidogo mwa njia ipitayo mlimani. Majembe haya yako matatu tangu zama za kale.Majembe haya yanayo maajabu haya:-• Majembe hayapati kutu• Majembe hayahamishiki• Majembe huongezeka umbo wakati wa masika na hupungua umbo kiangazi.• Majembe haya yanajilinda yenyewe.Katika suala la kujilinda yenyewe, mtu akichukua jembe moja au yote, mara atakapoanza kutembea kutoka mahali yalipo, huanza kusikia uzito wa majembe unazidi kadri anavyozidi kwenda mbali. Hali kadhalika, kifua chake mtu huyo hujaa hivyo kuathiri upumuaji wake. Mara moja mtu huyu hulazimika pasipo uchaguzi wa aina yoyote kuyarudisha majembe haya mahali alipoyatoa.Mshangao mwingine ni kwamba pindi wazo la kuyarejesha linapomjia na kuanza safari ya kurudi, mara kifua chake huanza kufunguka na majembe kupungua uzito wa awali. Basi, kadri atakavyokuwa anakaribia, ndivyo uzito utakapozidi kupungua. Akisha fika mahali yalipokuwa, uzito wa majembe unakuwa wa kawaida tu.Majembe haya daima yako nje tu, yananyeshewa mvua masika yote, lakini cha ajabu huwezi kuyakuta yakiwa na kutu. Ebu jiulize hii ni chuma ya aina gani isiyopata kutu. Hii ni chuma ya kawaida tu ambayo mababu zetu waliyeyusha mawe na kupata chuma ya kutengenezea majembe haya wakati wa Muhula wa Mawe.

Wakati wa kiangazi ni wakati mzuri wa kwenda kuyaona majembe haya na kubaini umbo lake la wakati huo. Wakati huu huwa yamepungua na kuwa madogo tofauti na wakati wa masika ambapo umbo lake hubadilika na kuwa makubwa. Hali hii huendelea hadi mvua zinapoanza kupngua na majembe nayo pia huanza kupungua maumbo yake.Maumbo haya huendelea kupungua mpaka kiangazi. Hali hubadilika tena pale miti inapoanza kuchipua ikiashiria ujio wa masika. Hivyo basi, maumbo ya majembe haya huendelea kukua hadi nyakati za kuanza kilimo. Majembe huionekana katika umbo lenye ukubwa mmoja wakati wa masika inapokuwa katikati. Hali hii huwa sawa na kiangazi kinapokuwa katikati wakati majembe haya yanapokuwa katika maumbo madogo ukilinganisha na masika.Majembe haya hayana ulinzi, bali hujilinda yenyewe. Hakuna mtu anayekuzaia kuyachukua, wewe yachukue lakini wewe mwenyewe utayarudisha mahali ulipoyatoa, wala haitawezekana ukayatupa popote. Suala la kuyatupa halitawezekana, kwani kifua chako hakitafunguka mpaka hapo utakapoyarejesha sehemu ulipoyatoa.Hakuna masharti yoyote yanamwongoza mtu kuyashika majembe haya. Majembe yanashikwa ama kubebwa pasipo sharti lolote, unatazama kadri unavyoweza kisha unarudisha mahali ulipolitoa kisha unaondoka.Maeneo mengine hutawaliwa na masharti, lakini eneo hili halina masharti yoyote
HISANI YA LUKWANGULE BLOG

No comments:

Post a Comment