.

.

.

.

Thursday, April 01, 2010

MCHAKATO WA KUMPATA MRITHI WA MAXIMO

NCHI za Ulaya zimeongoza katika kuwa na waombaji wengi kati ya waliojitokeza kuwania kazi ya ukocha mkuu wa timu ya taifa, Taifa Stars ambayo iliyotangazwa hivi karibuni na Shirikisho la Soka Tanzania TFF).
Akizungumza na waandishi wa habari leo katika ukumbi uliopo jengo la Millenium Tower, Kijitonyama, Dar es Salaam, Rais wa TFF, Leodegar Tenga alisema, maombi kutoka nchi za Ulaya ni zaidi ya nusu ya maombi yote ambayo alisema ni 59.
Tenga alisema, wakati Ulaya ikiongoza kwa kuwasilisha waombaji 48, waliojitokeza Tanzania ni watatu ukiacha mmoja ambaye aliomba ukocha msaidizi, nafasi ambayo Tenga alisema hakuna.
Alitaja nchi nyingine ambazo raia wake wametuma maombo kusaka nafasi hiyo kuwa ni Kenya, Cameroon na Ghana ambazo ameomba mmoja kila nchi, Mataifa ya Asia bila kutaja nchi kwa ujumla wameomba watatu na Amerika ya Kusini ikiwa imetoa wawili.
Tenga alisema, kwa sasa TFF haitataja wagombea hao, lakini alieleza kuwa wengi wa alioomba nafasi hiyo ni wenye uzoefu mkubwa katika masuala ya soka na kwamba mchakato safari hii utakuwa rahisi kutokana na kujitokeza idadi kubwa ikilinganishwa na mchakato uliopita ambao walikuwa watatu tu.
Alisema, kumiminika kwa idadi ya maombi kutaka kuinoa Stars inamaanisha kwamba Tanzania ipo kwenye chati nzuri na yenye kujulikana zaidi kisoka kuliko miaka iliyopita, kazi ambayo alisema imefikiwa kutokana na utendaji wa viongozi mbalimbali wa usimamizi wa mchezo huo nchini ikiwemo TFF.
Tenga alisema, hadi sasa tayari sekretairieti imeshafanya mchakato wake kuhakikisha wanaoitwa kweneye kinyang'anyiro ni idadi ile yenye waombaji wenye sifa za uhakika na si wale walioomba kwa ajili ya kubahatisha tu huku wakijijua hawana sifa za kitaaluma ukiachilia mbali uozefu ambao alisema wengi wanao.
Alisema, utaratibu uliowekwa unailelekeza TFF kuwa anayestahili kuionoa Stars lazima awe na kiwango cha elimu ya sekondari, lakini pia awe na cheti cha ngazi ya diploma ya mafunzo ya ukocha na siyo vyeti vingine kama vya Saikolojia na mazoezi ya viungo tu na kusema kuwa wengi wa waombaji wanazo diploma.
Tenga alisema wenye sifa hizo wameshapatikana na awamu iliyofuata ilikuwa kuwatumia maswali ambayo waombaji watatakiwa wawe wameshaleta majibu yao TFF kabla ya Aprili 15, 2010.
Alitaja maswali waliyotumiwa kuwa ni yanayolenga kujua mambo kadhaa kama mwombajianafanya kazi wapi kwa sasa, atapatikana lini akikubaliwa na kiwango cha mshahara anachotaka awe analipwa.
Tenga alisema baada ya majibu kuletwa, Kamati itakaa kujadili waliopatikana.
Nafasi ya Kocha Mkuu wa Taifa Stars imetangazwa kuwa wazi kufuatia kocha mkuu wa sasa Mbazil, Marcio Maximo kukaribia kumaliza mkataba wake.

No comments:

Post a Comment