.

.

.

.

Monday, July 02, 2012

RAIS KIKWETE ASEMA SELIKALI YAKE HAIHUSIKI .......

WAKATI Mwenyekiti wa Jumuiya ya Madaktari Tanzania, Dk Steven Ulimboka akiendelea na matibabu Afrika Kusini, Rais Jakaya Kikwete amesema Serikali haihusiki na kilichomtokea daktari huyo kwa kuwa alikuwa kiungo muhimu katika majadiliano baina ya pande hizo mbili.

Rais Kikwete alisema hayo jana katika hotuba yake ya kila mwezi, ambapo mbali na suala hilo, pia alizungumzia sababu za mgomo wa madaktari na usafirishaji wa wahamiaji haramu.

Dk Ulimboka ambaye alikuwa anaratibu mgomo wa madaktari unaoendelea nchi nzima kutokana na Serikali kushindwa kutimiza madai yao mbalimbali, anatibiwa figo na majereha aliyoyapata katika sehemu mbalimbali za mwili, baada ya kutekwa na watu wasiojulikana, kisha kupigwa, kung'olewa kucha, meno mawili na kutupwa katika Msitu wa Pande, usiku wa kuamkia Jumatano iliyopita.

Tangu kutokea kwa unyama huo uliofanywa na watu wasiojulikana, baadhi ya wananchi na wanaharakati wamekuwa wakiilaumu Serikali kuwa inahusika na utekaji huo na wengine wakienda mbali zaidi, kuwa watekaji walikuwa wanamlazimisha kueleza nani yuko nyuma ya mgomo wa madaktari.

Rais Kikwete, kama awali alivyosema Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, walisema wanatambua kuwa, Serikali nayo inatajwa katika orodha ya wanaotiliwa shaka kuhusu kilichomtokea Dk Ulimboka, lakini yeye ameshangazwa na hisia hizo, kwani haoni sababu ya Serikali kufanya hivyo.

"Dk Ulimboka alikuwa kiungo muhimu katika mazungumzo baina ya Serikali na madaktari. Ni kweli kwamba yeye si mtumishi wa Serikali, hivyo hakustahili kuwa sehemu ya majadiliano haya.  Kulikuwa na rai ya kutaka asiwepo, lakini nilisema wamuache maadam madaktari wanamwamini kuwa anaweza kuwasemea vizuri zaidi kuliko wao wenyewe walioajiriwa na Serikali," alisema Rais Kikwete.

Alisema Serikali haina sababu ya kumdhuru Dk Ulimboka kwa sababu suala la mgomo, Mahakama Kuu imekwishatoa amri ya kuusitisha, hivyo anayekaidi amri hiyo atakuwa ananunua ugomvi na mhimili huo wa dola, ambao wenyewe una mamlaka ya kumtia adabu.

"Hivi baada ya kufika hapo Serikali iwe na ugomvi na Dk Steven Ulimboka kwa sababu ipi na jambo lipi hata iamue kumdhuru?" alihoji na kuongeza:

"Kama kuna mtu wa Serikali kafanya, itakuwa kwa sababu zake binafsi na siyo za Serikali au kwa kutumwa na Serikali," alisema Rais Kikwete.

Alisema alichofanyiwa Dk Ulimboka kimemsikitisha na kumhuzunisha kwa kuwa ni kitendo cha kinyama na kinyume kabisa na mila na desturi za Tanzania.

Alisema Watanzania hawajazoea mambo hayo na kwamba ameelekeza vyombo vya ulinzi na usalama kufanya uchunguzi wa kina ili ukweli ujulikane.

No comments:

Post a Comment