.

.

.

.

Thursday, August 02, 2012

LISA JENSEN AANZA KUPETA MISS WORLD 2012



MWAKILISHI wa Tanzania katika mashindano ya Miss World, Lisa Jensen ameanza kufanya kweli katika michuano hiyo baada ya kufanikiwa kuingia kumi bora ya shindano la Top Model, hivyo kumuongezea pointi zaidi kabla ya fainali za kinyang’anyiro hicho.


Habari zilizopatikana kutopka Mongolia ambako shindano la Miss World litafanyika, zimepasha kuwa Lisa alikuwa mwiba mchungu kwa washiriki wengine kutokana na uwezo wake mkubwa, huku akionesha kipaji cha aina yake katika shindano hilo lililofanyika juzi usiku nchini humo. Akithibitisha habari hizi, Afisa Habari wa Kamati ya Miss Tanzania, Haidan Ricco alisema Lisa ni mmoja kati ya wawakilishi watatu kutoka Bara la Afrika ambao wamefanikiwa kupenya na kuingia katika nafasi hiyo muhimu.

Waafrika wengine waliofanikiwa kupenya katika kumi bora ya shindano hilo kabla ya siku ya fainali ya Miss World ni mrembo wa Afrika Kusini na Shelisheli. Lisa amefanikiwa kufanya kweli na kuwatoa kimasomaso Watanzania ambao kwa sasa wanajikuta katika hali mbaya kutokana na wanamichezo wake waliopo katika Michuano ya Olimpiki wakifanya vibaya.

Kutokana na kuingia kumi bora, Lisa bado ana kazi kubwa ya kuhakikisha anapambana ndani ya wiki hii wakati mshindi wa Top Model atakaposakwa rasmi. “Kwetu sisi ni faraja kubwa mno, kwani tunaamini Lisa ataiwakilisha vema Tanzania na huu ni mwanzo mzuri kwake,” alisema Ricco, huku akitaka Watanzania wamuombee kabla ya kufanyika shindano la Miss World hapo Agosti 18, ili aweze kufanya kweli.

Shindano la Miss Tanzania kwa sasa linadhaminiwa na kinywaji cha Redd’s, ambacho kinazalishwa na Kampuni ya Bia Tanzania.

1 comment: