.

.

.

.

Monday, August 20, 2012

UMRI WA KUINGIZA MAGARI TANZANIA KUBAKI MIAKA 10

Pendekezo la serikali kutaka kupunguza umri wa magari unaoingia nchini uwe wa miaka minane kutoka miaka 10, limekwama.

Pendekezo hilo liliibua mvutano mkubwa bungeni jana, baada ya wabunge kulipinga na kusababisha Waziri Mkuu, Mizengo Pinda kuingilia kati.
Mvutano uliibuka wakati serikali ilipowasilisha muswada wa sheria ya fedha utakaowezesha ukusanyaji wa mapato kwa mwaka 2012/13 kwa lengo la kufanikisha utekelezaji wa bajeti yake.
Akiwasilisha muswada huo, Waziri wa Fedha William Mgimwa, pamoja na mambo mengine, alisema serikali inakusudia kupunguza muda wa magari yaliyotumika kuingia nchini ili kudhibiti magari chakavu, kutunza mazingira na kuwapunguzia wananchi mzigo wa kununua mafuta kwa kuwa yanatumia nishati hiyo kwa wingi.
Alisema serikali inatekeleza hoja hiyo kwa kuwa hata Kenya na Uganda wameanza kufanya hivyo na kwamba ni mpango wa  nchi nyingi.
Baada ya kuwasilisha muswada huo, Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Fedha na Uchumi, iliwasilisha maoni yake na kupinga pendekezo hilo la serikali kwa kueleza kwamba uwezo wa wananchi wengi kununua magari mapya ni mdogo hivyo pendekezo hilo litawaumiza.
Akiwasilisha maoni ya kamati, Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Andrew Chenge, alisema serikali pia haina nia ya kuyaondoa barabarani magari yenye umri zaidi ya miaka 10 hivyo pendekezo hilo halina manufaa kwa taifa.
“Kamati ina amini kwamba sababu zilizofanya serikali kuleta mapendekezo bungeni mwaka 2006 ya kutoza ushuru wa bidhaa za magari yenye umri zaidi ya miaka 10 bado zina nguvu hadi leo…kamati inashauri umri wa magari yanayostahili msamaha uwe miaka 10 na sio minane inayopendekezwa,” alisema.
Msimamo huo wa Kamati uliungwa mkono na Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, ambayo ilisema hoja ya serikali katika eneo hilo ni dhaifu kwa kuwa wananchi wengi hata wabunge hawana uwezo wa kununua magari mapya na wala umri wa gari sio kigezo pekee cha ubora.
Akiwasilisha maoni ya kambi hiyo, Mbunge wa Viti Maalum (Chadema), Christina Mughwai, alisema inashangaza serikali inaleta mapendekezo hayo miezi michache baada ya kuleta muswada wa kuiruhusu kununua vyombo ‘chakavu’ vya usafiri ambayo imepitishwa na Bunge.
Baada ya msimamo huo, Bunge lilikaa kama kamati kwa ajili ya kupitia kifungu kwa kifungu ili kupitisha muswada huo, lakini wabunge hususani wa CCM akiwamo Peter Serukamba (Kigoma Mjini na Christopher Ole Sendeka, waliungana na kamati pamoja na kambi ya upinzani.
Akijibu, Waziri Mgimwa alisisitiza kwamba azma hiyo inalenga kulinda mazingira na kuwasaidia wananchi wanaotumia magari kwa kuwapunguzia mzigo wa kununua mafuta kwa kuwa magari chakavu yanatumia mafuta mengi.
Kadhalika, Mgimwa alisema magari chakavu yanachangia kuongeza ajali.
Majibu hayo yaliibua hasira za wabunge ambao walimpinga walieleza kuwa magari chakavu sio pekee yanayochafua mazingira kwa kuwa ukataji miti kwa ajili ya mkaa ni eneo linalochangia zaidi uharibu wa mazingira nchini.
Mvutano huo ulimlazimu Waziri Mkuu Pinda kuingilia kati na kueleza kwamba serikali imekubaliana na maoni ya wabunge na kukubali umri wa magari yanayoingia nchini uwe miaka 10.
Hata hivyo, Pinda aliwataka wabunge wafanye utafiti zaidi juu ya athari za magari chakavu ili ikiwezekana baadae wazo hilo la serikali liridhiwe na Bunge.

No comments:

Post a Comment