.

.

.

.

Thursday, August 01, 2013

AOMBA KATIBA MPYA IRUHUSU RAIS KUSHITAKIWA

 Mwanasiasa mkongwe nchini, Mateo Qaresi ambaye amewahi kushika nyadhifa mbalimbali katika Serikali ya Awamu ya Pili na Tatu, ikiwamo uwaziri na ukuu wa mkoa, amesema Tanzania kama taifa halina dira wala mwelekeo na matokeo yake mambo yake yamekuwa yakienda bila utaratibu huku akishauri Katiba Mpya iruhusu Rais ashtakiwe.
Akitoa maoni kuhusu Rasimu ya Katiba Mpya jana, Qaresi ambaye ni Mjumbe wa Baraza la Katiba la Wilaya ya Babati amepinga mapendekezo mengi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) akisema ni muhimu Katiba Mpya itaje dira ya taifa.
Qaresi katika utumishi wake wa umma, amewahi kuwa Waziri wa Ushirika na Masoko kati ya mwaka 1989 - 1990, Waziri wa Utumishi, 1996 - 2000 na Mkuu wa Mkoa wa Mbeya tangu 2000 hadi Februari 2006.
“Hivi hawa viongozi wanajua tunapoelekea, leo hii ukiulizwa dira yetu ni nini hakuna anayejua, bali tunajiendea tu,” alisema.
Alisema kwa mfano, Wamarekani licha ya kuwa na vyama viwili vikubwa, lakini dira yao ni ubepari, Wachina au Warusi dira yao ni ujamaa (ukomunisti) na kwa mataifa yote yanazo dira, lakini Tanzania dira yake haijulikani.
“Basi, watangaze kama sisi ni mabepari, wajamaa au waliberali, ili tujue na tufuate misingi hiyo siyo kila kiongozi kuwa na utaratibu wake, wengine ruksa wengine hivi lazima tubadilike,” alisema Qaresi.

Rais aondolewe kinga, ashtakiwe
Akizungumzia ibara ya 83 ya Katiba ambayo inazungumzia kinga za Rais, alisema ni muhimu sasa kuondolewa kwani marais wamekuwa na viburi , hawashauriki.
Alisema kuna makosa ambayo marais wanayafanya ambayo yanafaa kushtakiwa, lakini kutokana na kuwa na kinga, imekuwa ni vigumu kufanya hivyo.
“Katiba ijayo lazima sasa iondoe kinga kwa marais ili mtu yeyote aweze kumshtaki Rais na hatua za kisheria ziweze kuchukuliwa,” alisema Qaresi.


Kuhusu hoja za Kundi la G55 ambalo yeye alikuwa mwasisi na mwanachama la kutaka Serikali ya Tanganyika, alieleza kuwa Serikali tatu haziwezi kuepukika na kuwataka wanasiasa wakiwamo wa CCM kuacha ushabiki.

No comments:

Post a Comment