.

.

.

.

Wednesday, September 11, 2013

MUSWADA WA KUPAMBANA NA MADAWA YA KULEVYA

Habari kwamba Serikali inaandaa Muswada wa aina yake wa Kuzuia na Kupambana na Dawa za Kulevya nchini hakika ni za kutia moyo. Tunasema zinatia moyo kutokana na Muswada huo kupendekeza uundwaji wa taasisi itakayopewa meno na madaraka kamili kupambana na biashara ya madawa hayo. Kama sote tunavyofahamu, biashara hiyo ya dawa za kulevya imepanuka kwa kasi ya kutisha na kuharibu maisha ya vijana wengi, mbali na kuchafua jina na taswira nzuri ya taifa letu mbele ya jumuiya ya kimataifa.
Katika miaka ya hivi karibuni, Tanzania imekuwa kichekesho cha dunia kutokana na Watanzania wengi kukamatwa kila kona ya dunia wakisafirisha dawa hizo. Ripoti ya Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Kupambana na Mihadarati na Uhalifu (UNODC), imesema Tanzania ni kinara wa kupitisha dawa za kulevya katika Ukanda wa Afrika Mashariki.
Takwimu zinaonyesha kwamba maelfu ya Watanzania wanashikiliwa katika magereza katika nchi nyingi duniani na wengine wengi wamenyongwa baada ya kutiwa hatiani na mahakama za nchi ambazo hazina chembe ya uvumilivu wa biashara hiyo, ikiwamo China.
Ni vigumu kujua jinsi Tanzania iliyokuwa ikiheshimika sana duniani imebadilika ghafla na kuwa kinara wa dawa za kulevya. Haipiti siku bila kutangazwa habari za Watanzania kukamatwa wakiwa na shehena kubwa za dawa hizo katika sehemu mbalimbali duniani.
Jambo la kushangaza ni kwamba wanaokamatwa ni vijana wanaopewa dawa hizo na wafanyabiashara wakubwa ili kuzisafirisha, huku wafanyabiashara hao wakiendelea kutesa mitaani.
Pamoja na kusema kwa muda mrefu kwamba inayo majina ya ‘magwiji wa unga’, wakiwamo baadhi ya wafanyabiashara na wabunge, Serikali bado imeshikwa na kigugumizi kuwataja hadharani au kuwafikisha mbele ya sheria. Ndiyo maana tunasema hatua ya Serikali ya kuandaa Muswada huo wa aina yake ili kuunda chombo chenye meno ya kupambana na biashara hiyo hakika ni ya kupongeza.
Ni hatua ya kupongeza kwa sababu Serikali sasa inaonyesha utashi na dhamira ya kupambana na biashara hiyo. Ni kweli hatua hiyo imekuja ikiwa imechelewa sana kiasi cha tatizo hilo kuonekana kuizidi kimo, lakini tunaamini muundo, madaraka na meno kitakachopewa chombo hicho vitatosha kuiangamiza biashara hiyo haramu iwapo watateuliwa watendaji wenye uadilifu kukiongoza.
Ni habari njema kwamba Muswada unaotayarishwa unapendekeza chombo hicho kiwe huru, mbali na kuwa na vitengo vyake vyenye madaraka ya kufanya uchunguzi, kukamata watuhumiwa na kuwafungulia mashtaka bila kutegemea Jeshi la Polisi nchini. Chombo hicho kitakuwa na makazi ya pamoja na Mahakama Maalumu itakayoundwa kuendesha kesi hizo ambazo zitachukua muda mfupi kabla ya hukumu kutolewa. Hivi sasa kesi hizo zinachukua zaidi ya miaka 10 kumalizika.
Muswada huo unataka watakaopatikana na makosa wasiwe tena na uhuru wa kulipa faini. Mahakama nazo hazitaruhusiwa kutoa dhamana kwa watuhumiwa na dawa zitakazopelekwa mahakamani kama ushahidi zitaharibiwa mara moja, kinyume na sasa ambapo ushahidi huo unatunzwa kwa muda mrefu. Uzoefu umeonyesha kwamba dawa hizo hupotea au huchakachuliwa katika mazingira ya kutatanisha.
Tuna kila sababu ya kuwa na matumaini kwamba sasa kiyama cha wauza ‘unga’ kimewadia. Tunaipongeza Serikali kwa kuweka mbele masilahi ya taifa kwa kuandaa Muswada usio na simile katika kupambana biashara hiyo haramu na hatari.

No comments:

Post a Comment