.

.

.

.

Tuesday, April 26, 2016

COASTAL UNION NA YANGA LEO JIONI

HATIMA ya Yanga kufuzu fainali za michuano ya Kombe la Shirikisho la TFF (FA) inatarajiwa kujulikana leo baada ya kikao cha Kamati ya Mashindano kukutana.
Mechi ya nusu fainali kati ya Yanga na Coastal Union iliyochezwa kwenye Uwanja wa Mkwakwani Tanga mwishoni mwa wiki iliyopita ilivunjika katika dakika ya 110 baada ya wachezaji wa Coastal kukataa bao la pili la Yanga na kuanzisha vurugu zilizosababisha mshika kibendera namba mbili Charles Simon kupasuliwa jicho la kushoto kwa jiwe lililotupwa na shabiki.
Akizungumza na gazeti hili jana, Kaimu Mkurugenzi wa mashindano wa TFF, Jemedari Said alisema wanasubiri ripoti ya Kamisaa na mwamuzi ndipo watoe maamuzi. “Jambo kama hilo likishatokea ni lazima kamati ya mashindano ikutane, kuangalia sheria na kanuni zinasemaje kabla ya kutoa maamuzi,” alisema.
“Taarifa tayari tunazo, ripoti zote zinatarajiwa kuwasilishwa ofisini leo hii (jana) na kisha kamati chini ya Mwenyekiti Geofrey Nyange ‘Kaburu’ itakutana haraka iwezekanavyo kuamua,” alisema Said.
Katika mechi hiyo Coastal Union iliyoonesha soka safi ilipata bao la kuongoza kupitia kwa kiungo wake Youssouf Sabo na Yanga ilisawazisha kupitia kwa mshambuliaji wake Donald Ngoma.
Dakika 90 za mechi hiyo zilimalizika bila kupata mshindi na ndipo ilipoamuliwa timu ziende muda wa nyongeza wa dakika 30, ambapo dakika za mwanzoni tu Amisi Tambwe aliifungia Yanga bao la pili na ndilo lililozua kizaazaa, ambapo Coastal ilidai Tambwe alifunga kwa mkono.
Wakati uamuzi wa mechi hiyo ya Coastal Union na Yanga ukisubiriwa, Azam FC wenyewe tayari walitinga hatua ya fainali ya Kombe la FA baada ya kuifunga Mwadui ya Shinyanga kwa penalti 5-3, katika mchezo uliochezwa kwa dakika 120 na kutoka sare ya 2-2 kabla ya kupigiana matuta.

No comments:

Post a Comment