.

.

.

.

Sunday, May 15, 2016

WAZIRI MKUU AKIWA LONDON AZUNGUMZA NA WATANZANIA WAISHIO NCHINI UINGEREZA


T4
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akizungumza na Watanzania Waishio  nchini Uingereza  kwenye ubalozi wa Tanzania uliopo London Mei 14, 2014.   Kulia ni Waziri wa Mambo ya Nje, Ushirikiano wa Afrika ya Mashariki Kikanda na Kimataifa, Augustine Mahiga. Kushoto ni Kaimu Balozi wa Tanzania nchini Uingereza, Msafiri  Marwa .

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema Serikali imeamua kupambana na wala rushwa ili kiasi kidogo cha rasilmali kilicholengwa kiweze kuwafikia wananchi.
Ametoa kauli hiyo jana (Jumamosi, Mei 14, 2016) wakati akizungumza na Watanzania waishio Uingereza kwenye mkutano uliofanyika kwenye Ubalozi wa Tanzania jijini London, Uingereza.
“Jambo tuliloamua kuanza nalo ni kupambana na rushwa. Tumeamua kufanya hivyo ili kurudisha umoja na maelewano miongoni mwa Watanzania, tunataka tuibadili Tanzania ili iwe ni ya Watanzania wote… tumechoka kuambiwa sehemu fulani mradi umekamilika halafu ukienda kuangalia hukuti kitu na fedha ile haipo,” alisema huku akishangiliwa.
Akizungumzia zoezi la kusaka watumishi hewa, Waziri Mkuu alisema Serikali itawashughulikia wale wote waliohusika na zoezi hilo. “Wafanyakazi hewa wamefikia zaidi ya 10,000 na tumeokoa zaidi ya sh. bilioni 4.5 zilizokuwa zikipotea kila mwezi. Tukikamilisha zoezi la kusaka watumishi hewa, sasa tutataka kujua ni akina nani walikuwa wakipokea fedha hizo. Waliohusika tutashughulika nao,”  alisisitiza.
Alisema hivi sasa Serikali inalenga kuwa na watumishi ambao wanafanya kazi kwa uaminifu, uadilifu na uwajibikaji mahali pa kazi. “Hiki ndicho kipaumbele cha Serikali ya awamu ya tano na tena zoezi hili litakuwa endelevu”, alisema Waziri Mkuu.
Akizungumzia kuhusu ukuaji wa uchumi, Waziri Mkuu ambaye alikuwa London kuhudhuria mkutano uliojadili mapambano dhidi ya rushwa kwa niaba ya Rais Dk. John Pombe Magufuli, alisema lengo la Serikali hivi sasa ni kuona kuna ukuaji wa uchumi unaoenda sambamba na huduma zinazotolewa kwa wananchi.
Alisema viwanda vingi viliuzwa na watu waliovinunua wakageuza kuwa ni maghala ya kufugia wanyama. Sisi tunataka vifufuliwe ili teknolojia mpya na za kisasa zije Tanzania. Nafasi ya kuwekeza iko kwa Watanzania wote walioko nyumbani na ninyi mlioko nje,” alisema.
Alisema ardhi ipo ya kutosha na akawataka wawaalike marafiki zao waje kuwekeza nchini, ili mradi wawe ni watu makini, wenye nia ya dhati ya kuwekeza nchini na wenye mitaji na siyo madalali (middlemen). “Tunataka usindikaji wa mazao na bidhaa ufanyike nchini mwetu badala ya kupeleka mazao ghafi nje ya nchi, kwa njia hiyo tutakuwa pia tumezalisha ajira kwa watu wetu,” alisema.
“Kuna Watanzania wanaishi Botswana, Ujerumani na Poland wameshaleta wawekezaji nchini. Kwa mfano wa Poland wameleta mradi wa umeme katika vijiji vitani wilayani Ileje. Kwa hiyo ninyi endeleeni kuishi Uingereza lakini mhakikishe kuwa ukaaji wenu hapa, unaleta tija kule nyumbani. Kumbukeni Tanzania na muwe tayari kuihudumia Tanzania,” alisema.
“Serikali inaamini itanufaika na uwepo wenu hapa Uingereza. Muweke kipaumbele cha kuwekeza nyumbani na mkishindwa mtutafutie marafiki zenu. Mwenye uwezo andaa andiko la mradi halafu uwasiliane na Balozi ili akusaidie kutafuta wahusika kule nyumbani,” aliwaasa.
Akijibu swali kuwa ana maoni gani juu ya Bunge kutorushwa ‘LIVE’, Waziri Mkuu alisema hatua hiyo ilichukuliwa ili kuwawezesha watu kufanya kazi kama ambavyo kaulimbiu ya Mhe. Rais Magufuli ya Hapa Kazi Tu inavyosema.
“Bunge la Tanzania lilikuwa ni bunge pekee katika Jumuiya ya Afrika Mashariki na duniani ambalo lilikuwa likirushwa LIVE kuanzia asubuhi hadi usiku. Ina maana katika kipindi cha Bunge la bajeti, ambalo linaendeshwa kila siku kwa miezi mitatu, Watanzania nao wangekuwa LIVE kwa miezi mitatu,” alisema.
“Tulilazimika kujifunza kutoka kwenye mabunge mengine. Hivi hapa Uingereza mnaangalia Bunge live kila siku?” alihoji Waziri Mkuu na kujibiwa kuwa linarushwa LIVE kwa pipindi kisichozidi dakika 15 wakati wa maswali kwa Waziri Mkuu tu.
Akitoa ufafanuzi, aliwaeleza kwamba Bunge la Tanzania linarusha ‘LIVE’ kila siku asubuhi wakati wa maswali ya kawaida na Alhamisi asubuhi wakati wa maswali kwa Waziri Mkuu lakini mijadala yote hurekodiwa na kuhaririwa na kisha kurushwa kuanzia saa 8-9 mchana na saa 3-4 usiku kwa siku husika.
Kwa Watanzania wanaopenda kufanya kazi na wanapenda kufuatilia mambo ya Bungeni, walikuwa hawaoni LIVE coverage jwa sababu walikuwa kazini lakini sasa hivi wanaweza kufuatilia masuala ya bunge kwani muda wa jioni uliopangwa mtu anakuwa ametoka kazini na anaweza kuangalia televisheni akiwa nyumbani baada ya kutoka kazini.

No comments:

Post a Comment