.

.

.

.

Tuesday, May 12, 2009

BENKI YA WANAWAKE KUANZA BIASHARA MWEZI UJAO

BENKI ya Wanawake inatarajia kuanza shughuli zake Juni, mwaka huu, huku wanawake wakitakiwa kujitokeza kwa wingi kuwekeza. Benki hiyo iliyokuwa ikisubiriwa kwa hamu kutokana na kutarajiwa kuwakomboa wanawake na kuwawezesha kuingia kwenye ushindani wa kibiashara, itatoa huduma kwa watu wote bila kujali jinsia. Akizungumza na waandishi wa habari mjini Dar es Salaam, jana, Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto, Margaret Sitta, alisema benki hiyo itakuwa na kitengo maalumu kwa ajili ya kutoa elimu kwa wajasiriamali. Alisema kitengo hicho kitasaidia kuwahamasisha wanawake nchini kujiunga na benki hiyo, ili kujikwamua kwenye lindi la umasikini. Margaret alisema kuanzishwa kwa benki hiyo ni mafanikio makubwa kwa wanawake nchini na kwamba, wazo hilo liliibuliwa wakati wa maandamano miaka 10 iliyopita, mbele ya Rais mstaafu Benjamin Mkapa. “Ni wakati mzuri sasa kwa wanawake wote nchini kujiunga kwenye vikundi na kuwekeza katika benki yetu. Tutaweza kukuza SACCOS zetu, kwani wote tutaweza kununua hisa,” alisema. Tayari hisa za benki hiyo ambayo serikali imeipatia mtaji wa sh. bilioni 2.6 kati ya bilioni sita, zimeanzwa kuuzwa na kwamba, hisa moja inauzwa sh. 1,000 na zinapatikana wizarani.

No comments:

Post a Comment