.

.

.

.

Tuesday, December 30, 2014

MVUA YALETA KIZAIZAI BONGO

Mvua iliyonyesha kwa saa mbili katika maeneo mbalimbali ya Jiji la Dar es Salaam jana, imeleta kero kwa wasafiri wa vyombo vya moto na watembea kwa miguu na kusababisha baadhi ya barabara kushindwa kupitika kutokana na kujaa maji.
Mvua hiyo iliyoanza saa nne asubuhi hadi saa sita mchana, ilisababisha baadhi ya barabara kutopitika ikiwamo ile ya Samora karibu na Jengo la Wizara ya Nishati na Madini, baadhi ya maeneo ya Upanga na Msasani.
Aidha, watumiaji wa Barabara za Azikiwe, Bibi Titi na Morogoro katikati ya jiji walikuwa na wakati mgumu kupita, wengi walionekana wakiwa wamevua viatu au kutafuta njia mbadala kukwepa maji hayo ambayo yalionekana kuchanganyika na majitaka yaliyotokana na baadhi ya chemba kujaa.
Eneo linalojengwa njia za mabasi ya haraka katika eneo la Akiba, lilifunikwa na maji na kusababisha usumbufu kwa vyombo vya moto na watembea kwa miguu.
Maeneo ya Kariakoo, Barabara ya Uhuru na Msimbazi, yalijaa maji kama ilivyokuwa Barabara ya Umoja wa Mataifa na kuelekea Hospitali ya Taifa Muhimbili ambazo zilikuwa hazipitiki kutokana na mvua hizo na kusababisha msongamano mkubwa wa magari.
Wakazi wa mabondeni walianza kuingiwa na hofu ya kukumbwa na mafuriko wakati hali ya hewa ilipokuwa inabadilika huku mvua ikiongezeka kwa kasi. Katika bonde la Msimbazi, Kigogo na Jangwani wakazi walionekana wenye hofu baada ya mvua kuongezeka.
Mkurugenzi wa Jiji la Dar es Salaam, Wilson Kabwe alikataa kusema lolote na kusukuma mpira kwa Mkurugenzi wa Manispaa ya Ilala, Isaya Mgurumi.
Hata hivyo, Mgurumi alipopigiwa simu yake ya kiganjani ilikuwa inaita bila kupokewa.
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), Agnes Kijazi alisema hayo ni matokeo ya taarifa ya hali ya hewa waliyoitoa Oktoba, Novemba na Desemba ambayo yalibainisha kuwa kutakuwa na vipindi virefu vya jua katika msimu wa mvua pamoja na mvua kubwa. Alisema mvua zilizonyesha jana, zinanyesha mwisho wa msimu wa mvua kama ilivyotabiriwa kabla.
Kijazi alisema kesho (leo) wanatarajia pia mvua kubwa kutokana na kuwapo kwa mkandamizo mkubwa wa hewa katika pwani ya Madagascar.
“Kesho (leo) tutatoa taarifa nyingine ya hali ya hewa kwa kipindi cha miezi mitatu mingine, hivyo wananchi watumie taarifa hiyo katika mipango yao mbalimbali,” alisema mkurugenzi huyo.
CHANZO: NWANANCHI

No comments:

Post a Comment