.

.

.

.

Friday, June 19, 2015

JAJI MSTAAFU AVURUGA WAGOMBEA WENZAKE



Hatua ya Jaji Mkuu wa zamani wa Tanzania, Augustino Ramadhani kujitosa kuchukua fomu za kuomba kuteuliwa na CCM kuwania urais imewavuruga wagombea wenzake wa urais na kuibua mjadala mzito katika maeneo mbalimbali nchini.
Mitandao ya kijamii ilijaa mijadala inayohusu kuingia kwake katika kinyang’anyiro hicho, huku baadhi ya wapambe wa wagombea wakieleza wazi kukatishwa tamaa na mgombea huyo ambaye wasifu wake unaonyesha ana sifa za ziada zaidi ya baadhi ya wagombea.
Miongoni mwa hoja zilizoibuliwa ni sifa ambazo CCM huzitumia bila kuzitaja, hasa kile kinachoitwa zamu kati ya Bara na Zanzibar na nyinginezo, ikielezwa kuwa akihitajika mgombea kutoka Zanzibar kumrithi Rais Jakaya Kikwete, Jaji Ramadhani anaonekana kufaa zaidi.
Katika mijadala hiyo, wapo waliohusisha hukumu alizowahi kuzitoa akiwa Jaji na baadaye Jaji Mkuu kwamba zililenga kukibeba chama hicho tawala kwa sababu anaonekana alikuwa na mapenzi nacho siku nyingi lakini wengine walieleza kuwa hawaoni tatizo kwa jaji huyo ambaye ni Rais wa Mahakama ya Afrika ya Haki za Binadamu.
Jaji Ramadhani ajibu hoja
Wakati maoni ya wananchi yakitofautiana juu ya hatua ya Brigedia Jenerali huyo mstaafu kuchukua fomu, mwenyewe aliliambia gazeti hili jana kwamba kwa sasa si jaji tena, hivyo ana haki ya kugombea urais na hakuna kanuni wala sheria inayomzuia.
Alitoa ufafanuzi huo baada ya kuulizwa swali kuhusu Ibara ya 113A ya Katiba ya Tanzania inayotajwa kumzuia, ikisema; “Itakuwa ni marufuku kwa Jaji wa Mahakama ya Rufani, Jaji wa Mahakama Kuu, Hakimu wa ngazi yoyote kujiunga na chama chochote cha siasa, isipokuwa tu kwamba atakuwa na haki ya kupiga kura iliyotajwa katika ibara ya 5 ya Katiba.”
“Ukisoma Ibara hiyo inasema kama mhusika ni jaji. Mimi huko nimeshaondoka sasa nitashindwa kugombea kwa lipi? Wacha watu waibue mambo tu, lakini hata ukisoma Katiba utaona mwenyewe wao wanazungumzia past tense (wakati uliopita), sasa tunazungumzia present tense (wakati uliopo),” alisema.
Kuhusu mapenzi kwa CCM yanayoweza kuathiri utendaji, Jaji Ramadhani alihoji, “Hukumu gani niliipendelea? Hakuna kitu kama hicho. Kuanzia 1961 tulivyopata uhuru, majaji hawakuwa kwenye chama? Sasa kuna ajabu gani mimi kuwa katika chama maana kipindi hicho kulikuwa na chama kimoja tu, watu wote walikuwa katika chama si majaji tu.
“Zamani (wakati wa chama kimoja), ulikuwa huwezi kupata kazi ya aina yoyote kama wewe si mwanachama. Leo ajabu ni mimi tu. Hata wanahabari ilikuwa lazima wawe wanachama.”
Jaji Ramadhani ambaye alikuwa Makamu Mwenyekiti wa iliyokuwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, juzi mchana alichukua fomu kuwania nafasi hiyo ya kuongoza Serikali ya Awamu ya Tano huku akisema; chema chajiuza, kibaya chajitembeza.
Katika maelezo yake alisema alikuwa mwanachama wa Umoja wa Vijana wa Tanu tangu Agosti, 1969 wakati huo akiwa mwanafunzi wa Sheria katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam
.

No comments:

Post a Comment