.

.

.

.

Monday, April 04, 2011

VIGOGO WAZIDI KUTIA MGUU LOLIONDO

Waziri wa Nchi ofisi ya Rais (Uhusiano na Utaratibu) Steven Wassira na Mbunge wa Musoma vijijini Nimrod Mkono (kulia) wakinywa dawa kwa mchungaji Ambilikile Mwasapila katika kijiji cha Samunge, Loliondo wilaya ya Ngorongoro.Picha na Fidelis Felix

Neville Meena na Mussa Juma, Samunge
SAFARI za vigogo wa Serikali kwenda kijijini Samunge, Loliondo kwa Mchungaji Ambilikile Mwasapila kunywa dawa ya kutibu magonjwa sugu, zimeanza tena baada ya kusimama kwa siku kadhaa kutokana na kupungua kwa msongamano mkubwa wa magari uliokuwapo.Kupungua kwa foleni hiyo yapata siku mbili zilizopita, kumetoa fursa ya kuanza kwa utaratibu mpya wa kuruhusu magari machache yanayokwenda Samunge na jana safari za vigogo zilianza tena.

Waziri wa nchi, Ofisi ya Rais (Uhusiano na Uratibu), Steven Wassira na Mbunge wa Musoma Vijijini (CCM), Nimrod Mkono jana waliingia katika orodha ya vigogo ambao wamefika Samunge kwa Mchungaji Mwasapila kupata kikombe cha dawa ambayo inadaiwa kuwa tiba ya magonjwa sugu.

Machi 27, mwaka huu Serikali ilisitisha safari za magari kwenda Samunge sambamba na kuwataka vigogo waliokuwa wakitumia ndege na helikopta kutokwenda kijijini hapo hadi foleni ya magari iliyokuwapo itakapopungua.

Mkuu wa Wilaya ya Ngorongoro, Elias Wawa Lali aliliambia Mwananchi kuwa walikuwa wamewaomba mawaziri na viongozi wengine wa ngazi za juu kutopanga safari za kwenda Loliondo kwa Babu bila kuwasiliana na uongozi wa Serikali wa wilaya, lengo likiwa ni kudhibiti msongamano mkubwa uliokuwapo.

Msongamano wa magari ulikuwa ukisababisha mateso kwa watu waliokuwa wakienda kupata dawa na baadhi ya wagonjwa wafariki dunia wakiwa kwenye foleni hiyo na wengine iliwachukua kati ya siku saba hadi kumi na moja kufika kwa Mchungaji Mwasapila kupata dawa.

Wassira na Mkono wote wakiwa wabunge kutoka mkoani Mara, walifika Samunge majira ya saa nane mchana wakiwa kwenye gari la pamoja na kwenda moja kwa moja kwenye kibanda cha kutolea dawa na kila mmoja alipata kikombe cha dawa hiyo.

Akizungumza baada ya kupata dawa hiyo, Wassira alisema tiba inayotolewa na Mchungaji Mwasapila ni ya iana yake, si Tanzania tu, bali dunia nzima.

"Mimi nasema hapa ni mahali pa aina yake, katika nchi yetu na hata kwingineko duniani sijawahi kuona kiasi kikubwa cha watu wakikimbilia sehemu moja kupata tiba kama hapa," alisema Wassira na kuongeza:

"Wapo mamia ya Watanzania hapa na nimeambiwa hapa watu walikuwepo kwa maelfu. Lakini pia wapo watu wanaotoka nje ya nchi kuja hapa si jambo la kawaida... Nasema hili ni tukio la aina yake, si la kawaida tena si Tanzania tu, bali hata duniani kote," alisema.

Alisema mbali na majukumu ya kikazi yaliyomfanya kufika Samunge, lakini pia ametumia fursa hiyo kunywa dawa kama ambavyo mamia kwa maelfu ya Watanzania wamekuwa wakifanya.

"Watu wote wanakunywa dawa, kwa nini mimi nisinywe? Nimepata kikombe cha dawa, hilo siyo siri ijapokuwa muhimu ni mambo mawili makubwa ambayo yamenisababisha kufika hapa," alisema Wassira.

Alisema akiwa Waziri mwenye dhamana ya uhusiano wa jamii alilazimika kufika Samunge kuona jinsi watu wanavyoweza kuhimili mazingira hayo ambayo ghafla yamekuwa na watu wengi kwa wakati mmoja na bila kutarajia.

CHANZO :MWANANCHI

No comments:

Post a Comment