.

.

.

.

Saturday, April 13, 2013

TEKNOLOJIA YA MAGOLI KUANZA KUTUMIKA HAPA UINGEREZA MWEZI WA NANE MWAKA HUU



Klabu za ligi kuu soka nchini England zimepitisha sheria ya kutumia teknolojia ya camera katika maamuzi ya mchezo wa soka kuanzia msimu ujao.
 Kampuni ya Uingereza ya Hawk-Eye imeshinda tenda na kupatiwa mkataba wa kufunga vifaa maalumu kwenye viwanja vyote 20 vya timu za ligi kuu nchini England.

 Hawk-Eye itafunga kamera saba kwenye kila goli maalumu kwa kutambua kama mpira umevuka mstari wa goli na kumjulisha mwamuzi wa mchezo huo kupitia saa yake ya mkononi,na imesema inauhakika hakuna marejeo yoyote ya matangazo ya picha ambayo yatapingana na maamuzi ya teknolojia hiyo.
 Kampuni hiyo ya Hawk-Eye inajulikana kwa kufunga teknolojia kama hiyo kwenye mchezo wa Tenesi na Kriketi,ambapo camera maalumu huweza kutambua iwapo mpira umegusa mstari ama la na kumjulisha mwamuzi na wasaidizi wake ndani ya sekunde chache.
 Chama cha soka nchini England FA,kitafunga vifaa hivyo kwenye uwanja wa Wembley tayari kwa kutumika kwenye mchezo wa ngao ya jamii hapo mwezi wa nane mwaka huu.
 Vilabu vikubwa vyote nchini England vimepiga kura ya kupitisha maamuzi hayo katika mkutano wao uliofanyika hii leo jijini London,Huku viwanja vingine vya timu 17 zitakazosalia ligi kuu na zile 3 zitakazopanda daraja vitawekewa teknolojia hiyo na shughuli nzima itachukua wiki sita kukamilika.

 Msukumo wa kutumia teknolojia maalumu ya kutambua goli ilipata nguvu baada England kukataliwa goli lao la kusawazisha walipocheza na Ukraine,Mchezo ambao England walifungwa bao moja kwa bila kwenye michuano ya kombe la mataifa barani Ulaya mwaka 2012, Ambapo mwezi mmoja baadaye bodi ya vyama vya soka vya kimataifa (IFAB) katika kikao chake mjini Zurich kilipitisha teknolojia mbili ili zitumike kwenye michezo ya soka.

 Nalo shirikisho la kandanda Ulimwenguni FIFA kupitia kwa rais wake Sepp Blater alisema kukataliwa kwa goli la Frank Lampard kwenye mechi ya robo fainali kati ya England na Ujerumani mwaka 2010 katika michuano ya kombe la dunia,kulichangia kwa kiasi kikubwa maamuzi ya shirikisho hilo kupitisha sheria ya matumizi ya teknolojia ya kutambua goli.

Chama cha soka cha England kimesema kingependa kuona teknolojia hiyo inaanza kutumika kwa vitendo haraka iwezekanavyo.

No comments:

Post a Comment