.

.

.

.

Tuesday, January 06, 2015

WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA BA MAENDELEO YA MAKAZI NJIANI ......

Wakati wowote Rais Jakaya Kikwete anatarajia kuipanga safu mpya ya Baraza la Mawaziri kwa kuteua waziri mwingine wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi baada ya kumwondoa aliyekuwepo, Profesa Anna Tibaijuka.
Mara nyingi katika uteuzi wake Rais Kikwete amekuwa na utaratibu wa kuwapandisha baadhi ya naibu mawaziri kuwa mawaziri, kuwapa uwaziri wabunge ambao amewateua au kuteua waziri kutoka katika mkoa ambao anatokea waziri aliyeondolewa.
Profesa Tibaijuka ambaye ni Mbunge wa Muleba Kusini mkoani Kagera anakuwa waziri wa tatu kutoka mkoa wa Kagera kuondolewa madarakani katika uwatala wa Rais Kikwete. Ameondolewa  kutokana na kukabiliwa na kashfa ya uchotaji wa fedha katika Akaunti ya Tegeta Escrow.
Wengine walioondolewa kutoka mkoa huo ni aliyekuwa Waziri wa Maliasili na Utalii, Balozi Khamis Kagasheki kutokana na kushindwa kuwajibika  katika utekelezaji wa Operesheni Tokomeza Ujangili pamoja na aliyekuwa Waziri wa Nishati na Madini, Nazir Karamagi aliyeondolewa kutokana na sakata la Richmond.
Iwapo Rais Kikwete atazingatia utaratibu wake wa kuteua waziri kutoka mkoa ambao waziri aliyeondoka anatoka, huenda nafasi iliyoachwa wazi na Profesa Tibaijuka kuchukuliwa na  Charles Mwijage (Muleba Kaskazini), Gosbert Blandes (Karagwe).
Assumpter Mshama (Nkenge), Jasson Rweikiza (Bukoba Vijijini), Eustace Katagira (Kyelwa), Deogratius Ntukamazina (Ngara) na Dk Antony Mbasa (Biharamulo Magharibi).
Kama akitumia utaratibu wa kumpandisha naibu mawaziri, huenda nafasi hiyo ikachukuliwa na  Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, George Simbachawene ambaye ni Mbunge wa Kibakwe au naibu mawaziri kutoka wizara nyingine kama alivyowahi kufanya mara nyingi.
Kwa mujibu wa Ibara ya 66 (1) (e) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977, kama ilivyofanyiwa marekebisho inampa mamlaka Rais kuwateua wabunge 10, mpaka sasa ameshawateua wanane  na kubakiza nafasi mbili pekee.
Kati ya wabunge wanane walioteuliwa na Rais Kikwete, watano walipewa wizara za kuziongoza.
Wabunge hao na wizara zao kwenye mabano ni Shamsi Vuai Nahodha (Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa) na Profesa Makame Mbarawa (Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia).
Wengine ni Profesa Sospeter Muhongo (Nishati na Madini), na Saada Mkuya (Nishati na Madini) na Janet Mbene (Naibu Waziri Viwanda na Biashara) na Dk Asha-Rose Migiro.


Dk Migiro aliteuliwa kuwa Waziri wa Katiba na Sheria.  Wabunge ambao wameteuliwa na Rais, lakini hakuwapa uwaziri mpaka sasa ni Zakia Meghji na James Mbatia.

No comments:

Post a Comment