.

.

.

.

Wednesday, February 16, 2011

FEDHA BANDIA ZAINGIA KWENYE MZUNGUKO BONGO

KASHFA ya kukithiri kwa noti mpya bandia inazidi kuongezeka na sasa imebainika kuwa hata baadhi ya benki nchini zinashindwa kuzibaini na hivyo kujikuta zinaziingiza kwenye mzunguko.

Hali hiyo inatokana na Karani wa Fedha wa Kampuni ya Magazeti ya Serikali (TSN) Februari 14 kuchukua fedha benki ya CRDB tawi la Lumumba na bila kutambua hatimaye akagundua amepewa noti nyingi za Sh 10,000 zikiwa bandia.

Hata pale mmoja wa wafanyakazi wa TSN aliyepewa noti hizo alipokwenda kuweka baadhi ya noti hizo kwenye moja ya benki bila kujua kuwa ni bandia, karani wa benki hiyo alizipokea na kuzipitisha kwenye mashine na kuridhika kuwa ni halali.

Kitendo hicho kinaonesha kuwa mashine za benki hazizitambui noti hizo na hata wafanyakazi wenyewe wa benki yawezekana hawana utaalamu wa kutosha wa kutofautisha noti bandia na halali hasa za Sh 10,000.

Noti hizo ziligunduliwa na wafanyakazi waliopewa fedha hizo baada ya kuanza kuzitumia na kukataliwa mitaani ambapo jana baadhi yao walijikuta wakiwa na noti hizo.

Meneja wa Fedha wa TSN, Diana Lyatuu, alithibitisha kuchukuliwa fedha hizo kutoka benki ya CRDB tawi la Lumumba kwa kubadilishwa na hundi.

Noti nyingi ambazo zimezagaa ni zinazoishia na namba 366 na 362 ambazo ndizo wafanyakazi wengi wa TSN walikabidhiwa.

Mmoja wa wafanyakazi wa TSN, Nelly Mtema, alikamatwa na Polisi baada ya kuzitumia fedha hizo alizopewa ofisini kwa ajili ya kwenda kulipia bili ya maji katika ofisi za Kampuni ya Majisafi na Majitaka Dar es Salaam (DAWASCO).

Akielezea tukio hilo, Mtema alisema Februari 15 asubuhi alikwenda Dawasco kulipia maji lakini akashangaa kuwekwa chini ya ulinzi kwa maelezo kuwa ana fedha bandia.

“Niliwakatalia kuwa si bandia kwani nililipwa ofisini, lakini nikapelekwa Polisi kituo cha Kimara,” alisema Mtema ambaye baada ya kuzichunguza noti hizo aligundua bandia zikiwa tatu za Sh 10,000.

Aliongeza kuwa baada ya sakata hilo, alilazimika kupiga simu ofisini, kufahamisha kuwa fedha alizopewa ni bandia na amekamatwa na polisi baada ya kuzitumia kulipia huduma ya maji.

“Ofisini walizungumza na polisi juu ya kuwapo tatizo hilo ndipo nikaachiwa,” alisema Mtema.
Mkurugenzi wa Masoko wa CRDB, Tully Mwambapa, alipoulizwa juu ya tatizo hilo, alisema ana uhakika asilimia 100 ya fedha hizo hazikutolewa na benki yake.

“Sisi tuna sheria inayomtaka mteja ahesabu na ahakiki fedha zake kabla ya kuondoka dirishani, itakuwaje keshia aondoke ndipo tupokee malalamiko ya kuwapo fedha bandia?” Alihoji Mwambapa.

Keshia wa TSN alipoulizwa alisema hakuona haja ya kuhakiki fedha hizo kwa vile anaiamini benki hiyo kwani amefanya nayo kazi kwa siku nyingi. Hata hivyo, Mwambapa alisema: “Benki yangu ina sera ya kutoaminiana katika mambo ya fedha.”

Alijitetea kuwa kila dirisha lina kamera inayochukua mwenendo wa matukio ya kuanzia asubuhi hadi jioni yanayofanywa na karani aliyepo kwenye dirisha husika. “Ndiyo maana nasema fedha hizo hazikutoka kwetu,” alisema

No comments:

Post a Comment