.

.

.

.

Thursday, September 08, 2011

CHRISTINA SHUSHO .............


“UNIKUMBUKE Babaa unapowazuru wengine naomba unikumbuke, usinipite Yesu unapowazuru wengine naomba unikumbuke, unikumbuke babaa unapowazuru wengine naomba unikumbuke…”

Haya ni baadhi ya maneno yaliyomo katika moja ya nyimbo zinazomtambulisha vyema Mwimbaji wa Nyimbo za Injili, Christina Shusho.

Shusho amefanikiwa kujijengea sifa kwa mashabiki wa nyimbo za Injili ndani na nje ya mipaka ya Tanzania kutokana na nyimbo zake kubeba ujumbe mzito kwa jamii, lakini ukiwa katika msingi wa neno la Mungu ambalo analiamini.

Umahiri wake katika kuimba nyimbo za Injili umemuwezesha Shusho kutambulika vyema na kujinyakulia Tuzo mbalimbali ikiwemo Tuzo aliyopata wiki chache zilizopita huko Nairobi, Kenya.

Shusho alikuwa kati ya wasanii wa Tanzania waliopata Tuzo za Muziki za Afrika Mashariki na Kati (EMAS) zilizofanyika Agosti 20, mwaka huu na kushirikisha wasanii mbalimbali wa kutoka nchi nane za Afrika Mashariki na Kati.

Mwimbaji huyo aliibuka na Tuzo ya Msanii Bora wa Kike wa Nyimbo za Injili akiingia na wimbo wake Unikumbe na kumshinda mwimbaji mwenzake kutoka Tanzania Upendo Nkone aliyeingia na wimbo wake Haleluya Usifiwe, Alice Kamande kutoka Kenya na wimbo wake Upendo na Gaby kutoka Rwanda na wimbo wake Amahoro.

Wasanii wengine wa Tanzania walioshinda Tuzo hizo ni Bendi ya Muziki wa Dansi ya Msondo, Ambwene Yesaya `AY’ na Khamis Mwinjuma `Mwana FA’. Kutokana na ushindi huo, HABARILEO Jumapili lilipata fursa ya kukutana na kuzungumza na Shusho kuhusiana na ushindi huo, kazi yake, maisha yake na mafanikio aliyopata kutokana na uimbaji wake wa muziki wa Injili.

Akizungumzia Tuzo hiyo, Shusho ambaye ni mama wa watoto watatu anasema ni heshima kubwa kwa Mungu na kwake hasa kwa kuwa alishindanishwa na wanamuziki wenye vipaji vikubwa vya uimbaji wa nyimbo za Injili akiwemo mwimbaji mwenyeji Alice.

“Kidogo nilipata hisia za woga iwapo nitashinda hasa kutokana na ushiriki wa Alice ambaye ni mwimbaji mzuri wa nyimbo za Injili, lakini pia shindano lilifanyika nchini kwao hivyo mashabiki wake nilihisi kuwa ni wengi zaidi, lakini Mungu ni mwema nikapata mimi hiyo Tuzo hivyo nina kila sababu ya kumshukuru Mungu,” anasema.

Shusho anasema ushindi huo umemfanya ajisikie kumheshimu na kumnyenyekea zaidi Mungu kwa kumpeleka kila hatua, lakini pia anaona fahari kuwa watu ndani na nje ya mipaka ya Tanzania wanatambua kipaji chake na kazi aliyopewa.

“Naona ushindi huu mbali na kumheshimu Mungu zaidi, lakini pia naona nimepewa jukumu zaidi kwa maana kukitumia kipaji changu nilichopewa kwa kuimba zaidi ya hapa na kufikisha ujumbe kwa jamii kupitia uimbaji wa Injili,” anasema.

1 comment: