.

.

.

.

Tuesday, April 17, 2012

JAMES MILLYA AIHAMA CCM ............ AHAMIA CHADEMA

KITENDO cha Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM), Mkoa wa Arusha, James Millya kukihama ghafla chama hicho na kujiunga na Chadema kimekitikisa chama hicho tawala na jana kwa nyakati tofauti, viongozi wake walitoa matamko mbalimbali kumkejeli.

Mara tu baada ya Millya kutangaza kung'atuka CCM kwenye mkutano wake na waandishi wa habari mkoani Arusha, viongozi wa chama hicho, akiwamo Katibu Mkuu, Wilson Mukama, Katibu wa Uenezi na Itikadi, Nape Nnauye, Katibu Mkuu wa UVCCM, Martin Shigella, Makamu Mwenyekiti wa UVCCM, Benno Malisa, Katibu Mwenezi wa CCM Mkoa wa Arusha, Loota Sanare, walitoa matamko mbalimbali.

Kwa upande wake, Chadema kimefurahia hatua hiyo na jana Mwenyekiti wake, Freeman Mbowe aliwaambia waandishi wa habari mjini Dodoma kwamba kinampokea Millya kwa mikono miwili na kinaamini kuwa atakuwa na mchango mkubwa.

Jana, Ole Millya alitangaza kujivua nyadhifa zake zote ndani ya chama hicho tawala kuanzia ngazi ya taifa na kujiunga na Chadema akidai kuwa CCM kimefilisika kimawazo na hakitoi matumaini kwa Watanzania.

Akizungumza na waandishi wa habari Mjini Arusha jana, Ole Millya alisema amefikia uamuzi huo baada ya kugundua kuwa ‘gari’ alilopanda limepata pancha na haliwezi kumfikisha safari ya ukombozi wa taifa.

“Ukipanda gari halafu likapata pancha ambayo hakuna namna yoyote ya kuiziba na wala hakuna juhudi za kutafutia ufumbuzi tatizo hilo, busara ni kuhamia usafiri mwingine wenye uhakika wa kukufikisha safari yako,” alisema Millya.

Akirejea kauli ya Baba wa Taifa, Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, Millya alisema CCM siyo mama yake wala baba yake na kwa sababu kimeshindwa kujibu mahitaji na matatizo ya umma, ameamua kukihama.

“Natangaza rasmi kujitoa CCM na kujiunga Chadema kuendeleza harakati za kulikomboa taifa hili kutoka mikononi mwa watu wachache wenye fikra kwamba ndiyo wenye hatimiliki ya nchi hii,” alisema Ole Millya

Alisema amegundua kuwa alikuwa akichezea timu isiyo na uwezo wala nia ya ushindi katika ulingo wa siasa na uongozi wa umma na kujipa moyo kwamba licha ya kuchelewa kugundua kosa hilo, sasa amegundua na anakihama chama hicho kikongwe nchini.

Akiwa na wapambe wake wawili ambao hakuwa tayari kutaja majina yao kwa maelezo kuwa ni watu waliomsindikiza, alitaja mambo kadhaa yaliyomfanya akihame CCM ikiwemo kauli ya UVCCM mkoa wa Pwani waliodai Rais ajaye hawezi kutoka Mikoa ya Kanda ya Kaskazini.

“Baada ya kauli ile mimi nilitoa tamko kupinga na kulaani kauli hiyo kwa sababu ni kinyume cha katiba. Kanuni na taratibu za CCM lakini tangu kipindi hicho hakuna kiongozi yeyote ndani ya chama aliyejitokeza kukemea jambo hilo,” alisema Ole Millya.

Alisema licha ya kutangaza Rais ajaye kutotoka Kanda ya Kaskazini, vijana hao wa Pwani pia walidai anayemjua Rais wa Awamu ya Tano ni Rais Jakaya Kikwete akisema kitendo cha kiongozi huyo kukaa kimya ni kielelezo kuwa vijana hao walikuwa na baraka zake au za uongozi wa juu wa
CCM.

Ole Millya aliahidi kuwa kundi kubwa la vijana wa CCM wako nyuma yake na wanasubiri muda muafaka kuhamia Chadema.

No comments:

Post a Comment