.

.

.

.

Saturday, April 28, 2012

RAIS KIKWETE KUUNDA BARAZA JIPYA LA MAWAZIRI

RAIS Jakaya Kikwete, amewasilisha kwenye Kamati Kuu ya Taifa ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), taarifa yenye azma ya kulipanga upya Baraza la Mawaziri ili kuwawajibisha Mawaziri waliotajwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), kuhusika na ubadhirifu wa rasilimali za umma. 

Pamoja na Baraza la Mawaziri, Rais Kikwete katika taarifa hiyo kwa Kamati Kuu, ameeleza pia nia yake ya kupangua watendaji wakuu wa Wizara wakiwemo Makatibu Wakuu na watendaji wakuu wa taasisi na mashirika ya umma, waliotajwa pia na CAG kuhusika na ubadhirifu huo. 

Kutokana na kuibariki taarifa hiyo iliyowasilishwa na Rais Kikwete kwa Kamati Kuu, Dar es Salaam jana, Rais Kikwete ameshauriwa na Kamati hiyo kulisuka Baraza hilo mapema iwezekanavyo. 

Katibu wa Idara ya Itikadi na Uenezi ya CCM Taifa, Nape Nnauye aliwaambia waandishi wa habari kwamba pamoja na taarifa hiyo ya Rais, Kamati Kuu pia ilipokea na kuzijadili taarifa na maazimio ya Kamati ya Wabunge wa CCM na Kamati ya Uongozi ya Wabunge wa CCM juu ya kilichotokea kwenye Bunge lililomalizika hivi karibuni mjini Dodoma. 

“Pamoja na taarifa hizo Kamati Kuu imepokea taarifa ya jinsi Rais alivyojipanga kuchukua hatua za kuwawajibisha Mawaziri na Watendaji wa Serikali na wale wa mashirika ya umma waliobainika kuhusika na ubadhirifu ulioainishwa na taarifa ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa hesabu za serikali, Kamati za kudumu za Bunge na wabunge bungeni, “ alisema Nape. 

Alisema Kamati Kuu inatambua na kuheshimu haki na wajibu wa wabunge kujadili utendaji wa serikali yao na inapongeza juhudi za serikali kuhakikisha kuwa ripoti ya CAG inajadiliwa kwa uwazi na hivyo kuibua mapungufu yaliyojadiliwa na Bunge hilo. 

Kwa mujibu wa Nape, Rais Kikwete pamoja na kuhudhuria sherehe za Muungano, alikutana na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda juzi mchana, ambaye alimpatia taarifa ya kile kilichotokea bungeni Dodoma hadi kufikia hatua ya Kamati ya Wabunge wa CCM, kuwataka Mawaziri waliotajwa kwenye taarifa ya CAG kuwajibika.

No comments:

Post a Comment