.

.

.

.

Friday, May 25, 2012

CHUO KIKUU KIPYA TANZANIA KUANZA SEPTEMBA 2012

CHUO cha United African University of Tanzania (UAUT), kimekamilisha taratibu za kuanza kutoa masomo nchini na kitafanya hivyo kuanza mwaka ujao wa masomo. 

Sasa, chuo hicho kikuu kinachoendeshwa na Wamisionari kutoka Korea, kitaanza rasmi Septemba mwaka huu kwa kozi mbili za Shahada za Uhandisi wa Kompyuta na Teknolojia ya Mawasiliano ambayo itachukua miaka minne pamoja na Shahada ya Uongozi wa Biashara itakayochukua miaka mitatu. 

Naibu Makamu Mkuu wa Chuo hicho (Taaluma na Tafiti), Profesa Jo, Do Hyun aliwaambia waandishi wa habari Dar es Salaam jana kwamba chuo kiko tayari kuanza masomo na kwamba sasa kiko katika harakati za kusajili wanafunzi wenye sifa zinazotakiwa. 

“Tuko katika mchakato wa kusajili wanafunzi wenye sifa zinazotakiwa,” alisema Hyun na kuongeza kuwa kwa kuanzia, chuo hicho kitachukua wanafunzi 120, ambapo kila moja ya kozi hizo mbili itachukua wanafunzi 60. 

Alisema chuo hakitasajili wanafunzi kwa misingi ya dini zao, bali sifa za kitaaluma. Alisema kwa mwaka wa masomo unaoanza, chuo kitatoa ufadhili kwa wanafunzi 53 na watarajiwa wa ufadhili huo watatakiwa kuwa na vigezo vilivyowekwa. Ufadhili huo umewekwa katika makundi ya aina mbalimbali. 

Akielezea zaidi, alisema wanafunzi katika chuo hicho watapata fursa ya mafunzo kwa vitendo kwa muda wa miezi sita nje ya nchi na kwamba hiyo itasaidia kuwajengea mtazamo mpya wa dunia, kujifunza zaidi kivitendo pamoja na kujenga mtandao kwa faida yao na nchi kwa ujumla. 

Kwa mujibu wa mpango wa chuo hicho, mwaka 2013 utashuhudia kuanzishwa kwa Shahada ya Uhandisi wa Umeme na kwamba hadi kufikia mwaka 2015, shahada za Mawasiliano ya Jamii, Uandishi wa Habari, Famasia na Elimu ya Baioteknolojia zitakuwa zimeanzishwa. 

Profesa Hyun alisema wahadhiri kutoka maeneo mbalimbali duniani pamoja na kufanya mafunzo kwa vitendo nje ya nchi watasaidia kuzalisha viongozi bora wa dunia. 

Mwanzilishi wa UAUT, Mchungaji Joshua Lee alisema wanataka kuibua viongozi bora wa Kitanzania kupitia elimu watakayoipata watakaokuwa na upeo na busara. 

Alisema kutekeleza hili, watazingatia umuhimu wa taaluma ya kiwango cha juu, uhusiano mzuri na vyuo vingine, Serikali na taasisi za kitaifa na kimataifa

No comments:

Post a Comment