.

.

.

.

Saturday, May 31, 2014

BALOZI WA UINGEREZA ALETA KASHESHE

Serikali imetangaza rasmi mgogoro wa kidiplomasia kati yake na Balozi wa Uingereza nchini ikimtaka kujieleza kwa madai ya kuingilia mambo ya ndani ya nchi.
Mgogoro huo ulitangazwa bungeni mjini Dodoma jana na Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Steven Maselle aliyemtaka balozi huyo kufika Wizara ya Mambo ya Nje kujibu tuhuma hizo.
Kiini cha Serikali kumtuhumu balozi huyo ni hatua ya Mbunge wa Kigoma Kusini, David Kafulila (NCCR-Mageuzi) kuihusisha Uingereza na urejeshwaji wa Sh76 bilioni za chenji ya Rada.
“Katika mchango wake (Kafulila), ameongea jambo moja nyeti sana na hili bora niliseme ili liwe fundisho kwa wengine… Hii ni nchi huru baada ya mwaka 1961,” alisema Naibu Waziri.
“Zimekuwapo ripoti kwamba Balozi wa Uingereza amekuwa akijihusisha kuratibu vikao mbalimbali katika Jiji la Dar es Salaam na Dodoma kinyume cha utaratibu na hadhi ya kidiplomasia.”
Huku akionyesha kuwa na hasira, Maselle aliongeza kusema: “Vikao hivyo vina malengo ya kuhujumu mipango na mikakati ya maendeleo, ushahidi huo upo na utakapohitajika utatolewa.”
“Inasikitisha na kuchukiza balozi wa taifa kama Uingereza akifanya vitendo kinyume cha maadili… Anahusishwa kushawishi marafiki wa maendeleo wasitishe misaada ya kibajeti kwa Tanzania,”alisema.
Balozi wa Uingereza
Hata hivyo, Mwananchi ilimtafuta Balozi wa Uingereza Dianna Melrose, azungumzie suala hilo, msemaji wake Tamsin Clayton ambaye ni Mkuu wa Kitengo cha Siasa, Miradi na Mahusiano alisema wameshtushwa na taarifa hizo, lakini kwa sasa hawawezi kusema chochote mpaka wafahamu chanzo cha tatizo.
Aidha Naibu waziri Maselle alisema kuwa hivi karibuni Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP), alikuja Tanzania na kwamba upo ushahidi kuwa Balozi huyo wa Uingereza, alitamka kuwa anafikiria kuishawishi Serikali yake isitoe fedha za Miradi ya Maendeleo ya Millenia (MCC2).
“Ni aibu kwa Serikali ya Waziri Mkuu, David Cameron kwa balozi wake kufanya uwakala wa Benki ya Standard Chartered, kuishawishi Serikali ya Tanzania ikope fedha ili kulipa kampuni binafsi,” alisema Maselle huku akipigiwa makofi na wabunge wengi wa CCM na kuongeza:
“Rais Kikwete amelikataa kwa nguvu zote…, Serikali haiwezi kubeba mzigo wa kampuni binafsi.”

No comments:

Post a Comment